December 11, 2011
BANDARI WAACHIA BAISKELI ZA WALEMAVU
by Keneth Goliama
UONGOZI wa Bandari ya Nchi Kavu, iliyoko Kurasini jijini Dar es Salaam, imeyaachia makontena mawili ya baiskeli za walemavu uliyokuwa ukiyashikilia kwa miaka miwili sasa.
Hatua hiyo ilifanyika jana baada ya wabunge wanne kwenda katika bandari hiyo na kuomba makontena hayo yaachiwe ili kuwezesha baiskeli zilizoko ndani yake kusaidia walemavu wakiwamo wanafunzi wanaoshindwa kwenda shule kwa sababu ya kukosa usafiri.
Habari za awali zilisema makontena alipewa Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige, miezi kabla ya uchaguzi mkuu mwaka 2010, ili ayapeleke katika jimbo lake, lakini baadaye yalizuiliwa bandarini.Hata hivyo jana, wabunge wanne waliamua kufanya ziara ya kushtukiza katika eneo la bandari ya nchi kavu na kukutana makontena hayo yenye jumla ya baiskeli 1,100 yakiwa bado yamezuiliwa.
Baadaye waliuomba uongozi wa bandari, uruhusu makontena hayo yachukuliwe ili kuwezesha baiskeli zilizomo kutumika Wabunge hao walioongozwa na Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Philipo Mligo, Mwigulu Nchemba, Vick Kamata .
Makontena hayo yaliachiwa baadaya ya mbunge Nchemba kulipa Sh1.5 milioni, za ushuru wa kawaida.Hatua hiyo ilikuja baada ya wabunge hao kupiga magoti wakiomba msamaha wa kodi ili kuwezesha makontena hayo kuondolewa.Mligo alisema waliamua kufanya hivyo baada ya kuona idadi kubwa ya watoto wasiojiweza, wakiwa wanapata shida kwa kukosa baskeli wakati baskeli zikiwa zinaoza bandarini.
Alisema makontena hayo yaliyotolewa na Asasi isiyo ya Kiserikali ya Unit Diversity Foundation (UDF) na kwamba wameamua kuingilia kati ili kuhakikisha kuwa vifaa vilivyoko ndani yake vinanufaisha Watanzania. “Tunahitaji vitu vingi sana kutoka nje ya nchi lakini sisi wenyewe tunashindwa kunufaika navyo kutokana na ukiritiba ambao hauna hata msingi , kumbukeni hawa wahitaji hawakupenda kuwa hivyo,”alisema Mligo.Alisema asasi hiyo imekuwa ikitoa misaada ya baiskeli kwa walemavu na kwamba haifanyi biashara na kwa msingi huo wabunge baiskeli hizo zinapaswa kutolewa.
Kwa upande wake Nchema (CCM) alisema ameamua kutoa fedha zilizotakiwa ili kuhakikisha dhamira ya chama chake ya kuwasidia wananchi, inatekelezwa kwa vitendo."Sisi wabunge wa kawaida tunapaswa kuonyesha mfano katika kusaidia jamii, ni ajabu kuona vitu vinaoza wakati sisi tuna uwezo wa kuongea na kuhakikisha kuwa baiskeli hizi zinaachiwa,” alisema Nchemba.
Nchemba alisema asasi hiyo inafanya kazi nzuri ya kusaidia walemavu na kwamba, kwamba kwa sasa ilikua inakabiliwa na ukosefu wa Sh 150 milioni kwa ajili ya kulipia makontena hayo.Kwa upande wake, Kamata alisema alisema wanawake wanapaswa kuonyesha mfano katika kusaidia jamii .
Alisema walitarajia kuona wabunge wenye nia ya kusaidia jamii wanajitokeza katika kuomba vitu hivyo.Meneja Kitengo cha Makontena, Ally Kirro, alisema uamuzi wa kuachia makontena hayo umetokana na ombi la Serikali.